Saturday, February 6, 2016



 FALSAFA YA KIAFRIKA
Falsafa ni dhana ambayo haina namna moja ya kuifasili, wataalamu mbalimbali wametoa mawazo yao kuhusu dhana hii ya falsafa.

Wamitila (2003) anasema kuwa falsafa ni istilahi inayotumiwa kuelezea wazo au mawazo aliyonayo mtu au mwandishi. Mfano falsafa ya mwandishi inaweza kulenga mawazo ya mwandishi kuhusu maisha, mila, desturi, au utamaduni wa jamii husika atokayo mwandishi.
Sadipo (1993) anasema kuwa falsafa ni udadisi unaohusu dhana na kanuni zinazotuongoza kuhusu uzoefu au mazoea kuhusiana na maadili, dini, sheria, saikolojia, historia, sayansi za jamii, na siasa.
Kwa ujumla tunaweza kusema kuwa falsafa ni taaluma inayo dadisi hali halisi ya maisha ya binadamu kwa kuzingatia imani, mila, desturi, pamoja na mienendo aliyonayo binadamu katika jamii yake, huku akitafakari njia sahihi na bora za kuweza kutatua changamoto mbalimbali anazo kabiliana nazo katika maisha yake ya kila siku.
Kuhusu falsafa ya kiafrika wataalamu kama vile Placide Temples (1959), Oruka (1990), na Mbiti (2011). Wameifafanua dhana hii ya falsafa kuwa ni fikra au mitazamo wanayoishughulikia  waafrika wenyewe au watuwengine ambao wanakubali mila na desturi za kiafrika.
Kwa ujumla tunaweza kusema kuwa falsafa ya kiafrika ni dhana au mawazo ya waafrika juu ya mambo mbalimbali wanayoyafanya kama vile imani waliyonayo juu ya maisha, mila, desturi, namna ya kushirikiana katika katika jamii, na kutafuta suluhisho juu ya changamoto au matatizo yanayowakabili.
Vilevile kuna kuna sifa mathubuti zinazo itambulisha falsafa ya kiafrika, sifa hizo ni kama vile; falsafa ya kiafrika imejikita katika tanzu za fasihi simulizi, mfano visasili, visakale, sifo, ngano, mafumbo, vitendawili, miviga, ngomezi, tambiko, na ngoma.
Fasihi andishi; ni sanaa inayowasilishwa kwetu kwa maandishi. Hapa mkazo mkubwa hupo kwenye lugha, maandishi, na nyezo inayotumiwa kuiwasilisha au kuyawasilisha maandishi hayo. Fasihi andishi ni tokeo kuu la maendeleo ya jamii na kuvumbuliwa kwa mfumo wa maandishi (Wamitila, 2004).
Ni kweli kabisa kuwa falsafa ya kiafrika inajidhihirisha katika tanzu za fasihi simulizi na andishi ya Kiswahili. Kwa kuanza na fasihi simulizi ya Kiswahili, tanzu zifuatazo zinathibitisha hujidhihirishaji wa falsafa ya kiafrika miongoni mwa tanzu hizo ni kama zifuatazo;
Falsafa ya kiafrika inajidhihirisha katika hadithi; hadithi simulizi ni masimulizi ambayo yanatumia lugha ya mjazo au nathari na mtiririko wake huwa mwepesi au sahili (Wamitila, 2003). Kuna aina mbalimbali za hadithi simulizi kama vile ngano, visasili, visakale, hekaya, na nyingine nyingi. Kwa kiasi kikubwa falsafa ya kiafrika inajidhihirisha katika hadithi. Kwa mfano katika hadithi ya Fumo Aliongwe au Liyongo Fumo,
              “…Siku moja walikuwa msituni wakiwinda na wanawe. Harafu wakapumzika.      mwanawe akamuuliza naye akatoa siri ya kifo chake. Alisema kuwa yeye asingekufa isipokuwa       kwa kudungwa kwenye kitovu chake kwa sindano ya shaba…”
Kutokana na hadithi hii ni dhahiri kuwa waafrika wanaamini nguvu uhai kama anavyodokeza Placide Temples. Katika hadithi hii Fumo Aliyongwe aliweza kufa kirahisi baada ya kutolewa nguvu uhai. Vilevile katika hadithi ya ‘Rwanda Magere’ tunaona kuwa Rwanda Magere anategemea nguvu uhai zilizo katika kivuli chake. Hivyo kutokana na hadithi hizo ni dhahiri kuwa falsafa ya kiafrika hujidhihirisha katika hadithi simulizi.
Falsafa ya waafrika inajitokeza kupitia ushairi wa fasihi simulizi, waafrika wana mfumo maalumu wa fikra na hujishughulisha na mila, desturi, tamaduni, na namna ya kutatua matatizo yao. Katika wimbo wa Tom Malanga ulioimbwa na bendi (kundi) la Les Wanyika falsafa mbalimbali za kiafrika zimejidhihirisha kupitia wimbo huo. Dai hili linathibitishwa katika ubeti wa tatu (3) unaosema;
                “Tamaa ya maisha ndiyo chanzo cha maovu yote duniani.
                  Tamaa ikizidi mwisho wake husahau hata ndugu zako.
                 Sababu ya tamaa hujali hata wazazi wako.
                 Mkeo na watoto umewaacha na rafiki.
                Sababu ya tamaa umesahau amri za Mungu.
                 Kwamba usiue wala usiibe, usitamani vya watu.
                 Waheshimu baba na mama yako.
                  Tamaa mwisho ni majuto Ee wacha tamaa”
Msanii anadhihirisha waziwazi falsafa ya kiafrika anapozungumzia masuala ya ndoa, saula la dini, suala la maadili na suala la malezi ya familia. Hayo ni masula yaliyopo na yanayotokea katika jamii. Mwanafalsafa wa kiafrika “ Tempeles” anasema falsafa ya kiafrika imejikita katika mila, desturi, na tamaduni za kiafrika. katika wimbo huu kutokana na tamaa mbaya vijana wanakiuka maadili, hawawajali wazazi wao, wamewaacha marafiki, ndugu, wake, na watoto pia. Sababu ya tamaa wamesahau amri za mungu kuwa usiue. Usiibe, usitamani vya watu, pia waheshimu baba na mama yako. Mwisho wa tamaa ni kifo na kupelekwa gerezani. Hivyo basi msanii anaamini na anaonya kuwa mwisho wa tamaa ni majuto tuache  tamaa.
Falsafa ya kiafrika katika semi, semi ni tanzu ya fasihi simulizi ambayo hujishughulisha na maneno yasiyokua na majibu ya moja kwa moja kwa msikilizaji ama hadhira. Katika utanzu huu kuna vipera vinavyo ambatana nacho, baadhi ya vipera hivyo ni misemo, nahau, mafumbo, na lakabu. Semi ina dhima zake katika jamii inapotumika na baadhi ya dhima hizo ni kama vile kuelimisha jamii juu ya mambo mbalimbali mazuri ya kufanya, kama kufanya kazi kwa bidii, mfano msemo wa “asiyefanya kazi na asile”. Pia semi zina dhima ya kuonya na kuadabisha jamii juu ya mambo mbalimbali mabaya na yasiyofaa katika jamii, kama wizi, imani na tabia mbaya, mfano msemo usemao “mkaidi hafaidi mpaka siku ya idi”. Semi ni miongoni mwa tanzu za fasihi simulizi inayoonesha falsafa ya jamii moja na nyingine. Wanafasihi wana dhihirisha kuwa falsafa ya kiafrika inaweza kujidhirisha katika utanzu huu wa semi kwa kupitia vipera mbalimbali vya utanzu huu. Kwa  mfano, kupitia methali mbalimbali zinazotumika katika jamii ya waafrika dai hili linaweza kuthibitishwa,kwa kutumia mifano ya methali zifuatazo; “mwenye nguvu mpishe”, “Aungurumapo simba mcheza nani?”, na “Nazi haishindani na jiwe”. Kupitia methali hizi ni dhahiri kuwa falsafa ya Afrika inadhihirisha kuwa katika masuala ya utawala, waafrika walikuwa katika makundi madogo madogo kama vile koo au makabila, na mtu aliyekuwa anaaminika kuwa ni mwenye nguvu ndiye aliyekuwa anatawala katika jamii husika. Viongozi waliokuwa wanaaminika kuwa ni wenye nguvu ni kama vile; chifu Mkwawa, Kinjekitile Ngwale, na Chifu Mangungo wa Msovelo.
Falsafa ya kiafrika ikijidhihirisha katika sanaa za maonesho; katika kujadili vipengele vya ujidhihirishaji wa falsafa ya kiafrika, tumechagua vipera viwili katika utanzu huu ambavyo ni matambiko na ngoma.
Matambiko, ni kipera cha sanaa za maonesho ambacho wahusika wake katika jamii hufanya shughuli mbalimbali za kutoa sadaka kwa miungu, wahenga, na mababu waliowatangulia, ambao wanaonekana wana nguvu asilia zinazosaidia kuepusha utokeaji wa majanga kama njaa, radi, ukame, mafuriko, kuvamiwa au kutekwa kwa utawala, pamoja na kushinda vita. Katika jamii ya wasukuma, matambiko mbalimbali hufanywa ikiwemo matambiko yanayohusu kuzaliwa kwa mapacha (kulwa na doto) au kuzaliwa kwa mtoto aliyetanguliza miguu badala ya kichwa kama ilivyozoeleka (Ghashinje). Kwa upande wa mapacha wasipofanyiwa matambiko hatari inaweza tokea kama vile mvua kugoma kunyesha, mapacha hao kupigwa na radi na pengine kufariki dunia kabla ya kukua. Hii ina dhihirisha kuwa jamii ya wasukuma wanategemea nguvu ya ziada katika kukabiliana na majanga. Kwa upande wa mtoto anayezaliwa ametanguliza miguu, nae pia hufanyiwa matambiko ili aweze kuishi na kukua bila kupata matatizo. Shughuli mbalimbali wakati wa matambiko hufanywa mfano ngoma, nyimbo na sherehe zinazoambatana na wanyama kuchinjwa na damu zao kutumika kama sadaka kwa ajili ya matambiko hayo. Katika kuthibitisha hili Placide Temples anaeleza kuwa maisha ya jamii nyingi za wabantu wanategemea nguvu uhai (vital force) ili kujikinga na utokeajia wa majanga katika jamii hizo kama ilivyoneshwa katika jamii ya wasukuma.
Ngoma; hiki ni kipera kinachoonesha utokeaji wa falsafa ya kiafrika katika maisha halisi ya waafrika wenyewe. Ngoma katika jamii za kiafrika ni kiashiria cha mambo muhimu, mfano hutumika kama nembo ya utawala, kitumbuizi katika shughuli mbalimbali kama vile harusi au kupandishwa cheo. Katika jamii ya wasukuma ngoma huwa ni za aina mbili. Kuna ile inayochezwa katika shughuli mbalimbali kama vile harusi au matambiko na pia kuna ile ambayo inachezwa wakati wa kiangazi ambayo huusisha pande mbili, upande wa kwanza wanajulikana kama Bhaghika na upande wa pili ni Bhaghalu. Lengo kubwa ni kutumbuiza watu na kujua ubora wa “Manju” katika ngoma hizo. Pia ngoma hizo zina pande mbili zinazoshindana na hueandana na matumizi ya nguvu za asili (madawa ya kienyeji) ili kuwavutia watazamaji na kumuona Manju wa upande gani atakuwa bora zaidi ya mwenzake. Katika kujadili dhana ya falsafa ya kiafrika Temples anasema kuwa mwaafrika hawezi kuacha asili yake ambayo ndiyo utambulisho wa utamaduni wake. Kama ilivojidhihirisha  katika jamii ya wasukuma ngoma ni moja ya asili zinazotambulisha utamaduni wa jamii husika.
Baada ya kuangalia falsafa ya kiafrika inavyojidhihirisha katika tanzu za fasihi simulizi. Pia falsafa ya kiafrika inajidhihisha katika tanzu za fasihi andishi ya Kiswahili kama inavyoelezewa katika vipengele vifuatavyo;
Falsafa ya kiafrika inajidhihirisha katika ushairi; ushairi ni sanaa inayopambanuliwa kwa mpangilio maalumu wa maneno fasaha na yenye muwala, kwa lugha ya mkato, picha au sitiari au ishara katika usemi, maandishi au maadhi ya wimbo (Mulokozi na Kahigi, (1979). Kwa kutumia “Kunga za Ushairi na Diwani yetu” iliyoandikwa na Kahigi na Mulokozi falsafa ya kiafrika inajidhihirisha kama ifuatavyo;
Waafrika wanaamini katika suala la umoja; toka awali waafrika walikuwa na umoja waliishi kwa kushirikiana na hata kufa nya kazi pamoja kwa manufaa ya jamii nzima. Kwa kuumia shairi la “Msiba Uliotuangukia” suala la umoja kama imani ya waafrika linajidhihirisha;
                            “…Na mara shambulio tukalianza
                                 Huko sauti za chuki tunazipaza
                                 Tobaa litumbo la nduli kafiri
                                 Atakaye tumbole lituhasiri!
                                 Tukalichoma tukalikata sana…”
Shairi hili linaonesha kuwa waafrika waliamini katika umoja kama nyezo ya kupinga ukoloni na unyanyasaji. Pia waafrika wanaamini kuwa wazee ni watu wenye busara, hekima, na mawazo mazuri ambapo ni vyema kuheshimu mawazo yao. Mfano katika shairi lifuatalo;
                         “…Ndipo baina yetu utu umoja,
                               Mzee kidogo – maisha meonja,
                               Kutunyamazisha sote na kusema,
                               Tazama jama, janga limetuponza!
                                Lakini hivi hivi kukaakaa,
                                Pasipo kujaribu kujiokoa,
                                 Ni jambo la kijinga kupindukia…”
Suala la kifo; vilevile waafrika wanaamini kifo sio mwisho wa uhai bali ndio mwanzo wa maisha mengine. Waafrika wanaamini kuwa mtu akifa anaendelea kuishi kati yao ingawa hawamuoni. Hii injidhihirisha katika shairi la “Kwa MutwaMkwava na Mashujaa wengine” ambapo mtunzi anasema;
                    ‘…Shujaa Mkwawa hujafa waishi
                         Na sauti yako ingali aushi
                         Nasikia
                         Katika mpwito wa umma mapito
                        Nasikia
                        Katika nyimbo za watoto Soweto
                        Za wanyonge wapingao ubaguzi…”
Waafrika wanaamini kuwa watu walio kufa wapo karibu na Mungu na wale walio hai humuomba Mungu kupitia wale waliokufa. Hili linajidhihirisha kupitia urithishaji wa majina pamoja na matambiko  au kuomba mizimu ya mababu inayofanywa na waafrika wengi katika maisha ya kila siku.
Dhana ya uzuri na ubaya pia imejidhihirisha kama falsafa ya kiafrika hasa katika shairi la 19 “Wimbo wa Moyo” linalopatikana katika “Kunga za Ushairi”. Mtunzi wa diwani hii anadokeza kuwa uzuri au ubaya upo katika macho ya muonaji au anayeangalia, anasema;
                        “…Nimeamua kukuimbia leo
                         Jinsi wewe univutiavyo
                         Usooni tabasamu la huba;
                         Cheko lako ukicheka
                         Huniambukiza furahayo
                         Dodo mbivu matitiyo
                         Ni sherehe ya macho yaonayo
                         Na mikonayo yenye mbinu
                         Kiuno cha minenguo
                         Na macho ya uchawi
                         Konyezo la moyo uguswao
                         Hunitoa miayo ya hamu…”
Hii ni dhahili kuwa aghalabu uzuri au ubaya wa kitu kwa waafrika unategemea na mtazamo au mawazo ya muonaji. Hata katika jamii mtu anaweza kupenda au kukiona kitu fulani kizuri na mwingine kukiona kitu hicho ni kibaya.
Pia katika tamthiliya ya “Nguzo Mama” mwandishi ameonyesha falsafa mbalmbali ambazo zimezoeleka na zinatumika sana na jamii ya kiafrika. Falsafa zinazojidhihirisha katika tamthiliya hii, ambazo ni kama vile;
Dhana ya ngoma na nyimbo, katika tamthiliya hii mwandishi ameonyesha namna ngoma na nyimbo zinavyochukuliwa katika jamii nyingi za kiafrika. Ngoma na nyimbo huchukuliwa kama ni dhana ambazo zinazochochea umoja na ushirikiano kwa jamii wakati wa kufanya kazi na mara dhana hizi zinapokosekana kazi huzorota na hata watu huvunjika moyo na kushindwa kufanya kazi, na mwisho hutawanyika. Mwandishi “Penina Muhando” ametumia ngoma na nyimbo kama kichocheo cha kufanya kazi miongoni mwa wanawake wa Patata katika kuinua Nguzo mama kama inavyojitokeza katika ukurasa wa 44 na pia sehemu kubwa ya tamthiliya hii. Hivyo huu ni uhalisia uliopo katika jamii za kiafrika hususani kwenye makabila mbalimbali, ngoma na nyimbo huchukuliwa kama vichocheo na viashiria vya matukio ndani ya jamii.
Dhana ya mwanamke katika jamii, mwandishi Penina Muhando ameonyesha namna mwanamke anavyochukuliwa na jamii. Suala hili mwandishi amelizungumzia sana katika tamthiliya hii, kwani amewateua wanawake wa Patata namna wnavyojishughulisha na kazi mbalimbali katika familia zao na hata katika kuinua Nguzo mama huku akiwachora wanaume namna wanavyo wadharau wanawake kwa kushindwa kuinua Nguzo mama. Lakini pia namna wanaume wanavyowatesa wake zao, mfano Bi. Pili namna anavyojitahidi kuwahangaikia watoto wake huku mume wake akiwa ni mtu wa kunywa pombe na pale anaporudi nyumbani huishia kumpiga mke wake. Jambo hili lipo miongoni mwa jamii za kiafrika ambapo mwanamke anachukuliwa kama kiumbe duni asiyeweza chochote mbele ya mwanaume na ndio mitazamo ya wanaume na wazee katika familia nyingi za kiafrika,kwa mfano mtoto wa kike mara nyingi hutengwa na mtoto wa kiume katika shughuli mbalimbali likiwemo suala la elimu. Kwa hiyo mwandishi ameonyesha namna gani falsafa ya kiafrika inavyojidhihirisha juu ya anavyochukuliwa mwanamke, tofauti na Ulaya na Asia ambapo mwanamke amepewa nafasi kama mwanaume katika Nyanja zote  za kimaisha. Mwandishi katika ukurasa wa 36 anamuonesha Bi. Pili namna alivyojishughulisha na kuuza pombe ili aweze kuwatunza watoto wake, lakini bado anaonekana hafai mbele ya mume wake ambaye yeye kazi yake kubwa ni kuywa pombe na kumtukana mke wake, Bwana Sudi anasema
              “Kelele!Sasa mimi nitavaa nini. Utakausha kwa moto hiyo nakwambia. Mimi nataka kurudi nilikotoka nimeacha pombe kafiri. Unataka wenzangu wamalize? Kausha hiyo nguo kabla sijakupiga”.
Vile vile kupitia riwaya ya “Mirathi ya Hatari” iliyoandikwa na C. G. Mung’ong’o tunashuhudia falsafa ya kiafrika inajidhihirisha katika vipengele vifuatavyo kama ifuatavyo;
Suala la uhai na kifo, waafrika walio wengi mbali na kuamini kuwa vifo vingi vinavyotokea katika jamii vina sababu zake ambazo huelekezwa katika Mungu na uchawi au ushirikina. Haya yamezungumzwa na wanafalsafa wa kiafrika kama vile Placide Temples na Samweli Mbiti. Katika riwaya hii hali hii inajidhihirisha kupitia kifo cha mzee Kazumbe. Katika ukurasa (uk 37) inagundulika kwamba chanzo cha kifo ni kulogwa, mwandishi anasema “Mwanangu, leo asubuhi nilikwenda kwa mama Tumwene kuulizia kifo cha baba yako. Uganga unasema kuwa kifo chake kimetokea si kwa mapenzi ya Mungu, ila kwa michezo ya binadamu wafaidio kuwaona watu wakifa! Vile vile imesemwa mchezo haukwishia kwa marehemu wengine wetu watafuata hivi karibuni”. Huu ni uhalisia katika jamii zetu mbali na uwepo wa hospitali bado tunaamini nguvu za kiganga na kichawi.
Pia suala la dini, kupitia mwanafalsafa John Samweli Mbiti ni dhahiri kuwa waafrika wana dini zao tangu mwanzo mbali na ujio wa wakoloni ambao walileta  ukristo pamoja na uislamu wao. Katika riwaya hii mwandishi kupitia wahusika kama Gusto na mama yake (Nyamidze) ni wakristo tena huwa wana kwenda kanisani katika (uk 29) baada ya Gusto kuoga na kuvaa ili aende kanisani anamuuliza Nandi, “Hivi mama amekwenda wapi?” Nandi anajibu “Amekwenda kanisani”. Ni usiku huo huo tu wa kucha jumapili Gusto alihudhuria kikao cha wachawi mapangoni. Siku hiyo hiyo ya Jumapili mama yake Gusto (Nyamidze) anaenda kwa mganga (uk 37) kwa mama Tumwene. Huu ni uhasilia katika jamii zetu, matatizo yanapoikumba familia za watu mbalimbali miungu hukimbiliwa. Uamini kuwa mtu akifa hujiunga na miungu.
Suala la urithi, katika falsafa ya kiafrika tunaamini mzazi hasa baba anapofariki huwaachia urithi watoto wake hasa wa kiume. Urithi huo ni pamoja na mali za marehemu. Katika riwaya hii Gusto anarithishwa uchawi wa baba yake katika (uk 15) mwandishi anasema “Mwanangu na kuachia kazi kubwa. Ni urithi mkubwa ukiutumia vyema; bali pia ni mirathi ya hatari usipojihadhari nayo. Nakuachia dawa zote na milki yangu katika mizungu ya sihiri”. Mirathi hii anaipokea Gusto na baadaye inasababisha madhara makubwa ikiwa ni pamoja na vifo vya mama, dada, na hata kipenzi chake Dina ambapo vifo vimetokea kama kisasi baada ya Gusto kumtoa kafara mjomba wake Kapedzile. Suala hili la urithi lipo na linajidhihirisha katika jamii zetu za kiafrika.
Kwa kuhitimisha, tunaweza sema kuwa falsafa ya kiafrika imejikita hasa kuelezea mfumo mzima wa maisha anayoishi mwaafrika na ukweli kuhusu fikra, mila, utamaduni, na mienendo yake katika jamii. Kwa sasa falsafa ya kiafrika imeathiriwa kwa kiasi kikubwa na falsafa ya kimagharibi hususani suala zima la utandawazi. Waafrika taratibu wanasahau mila na desturi zao na kwa kiasi kikubwa kufuata na kuiga utamaduni na mwenendo wa maisha wa kimagharibi katika masuala mbalimbali kama vile, mavazi, vyakula (vyakula vya asili kama vile maboga, magimbi, viazi, pamoja na mihogo vina puuzwa kwa kiasi kikubwa na kizazi cha wakati huu), suala zima la dini, mfumo wa elimu na afya vyote vimebadilika kwa kiasi kikubwa kutokana na kuzuka kwa utandawazi. Pia maendeleo ya sayansi na teknolojia yamesababisha falsafa ya kiafrika kwa kiasi kikubwa kupotea, mfano ngoma za jadi katika kizazi hiki zinazidi kupotea kutokana na kuibuka kwa taaluma ya muziki kutoka katika iamii za kimagharibi.




                                                    MAREJEO.
Kahigi, K.K., & Mulokozi, M.M. (1979). Kunga za Ushairi na Diwani Yetu. Dar es Salaam: Tanzani Publishing House
Mbiti, J. (1990). African Religion and Philosophy. New York: Praeger Publisher
Muhando, P. (1982). Nguzo Mama. Dar es Salaam: Dar es Salaam University Press
Mung’ong’o, C.G. (1977). Mirathi ya Hatari. Dar es Salaam: Tanzania publishing House
Wamitila, K.W. (2003). Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus Publications







No comments:

Post a Comment